Kuhusu
Tuzo kwa Mahakama inaahidi kutoa tuzo ya hadi dola milioni tano kwa taarifa kuhusu shambulio la bomu la Ndege ya TWA 840. Mnamo tarehe 2 mwezi Aprili, mwaka 1986, bomu lililipuka ndani ya Ndege ya TWA 840 ilipokuwa safarini kutoka Roma, Italia, kuelekea Athens, Ugiriki. Mlipuko huo uliwaua raia wanne wa Marekani, akiwamo mtoto mchanga wa umri wa miezi tisa, mama yake, na bibi yake, wote ambao walitupwa nje ya ndege hiyo. Abiria wengine watano walijeruhiwa. Kwenye taarifa iliyotolewa mjini Beirut, Vikundi vya Kimapinduzi vya Waarabu vilidai kuhusika na shambulio hilo.

