Kuhusu
Tuzo kwa Mahakama inaahidi kutoa tuzo ya hadi dola milioni tano kwa taarifa kumhusu Abdelkarim Hussein Mohamed al-Nasser. Al-Nasser, anayedaiwa kuwa kiongozi wa shirika la kigaidi la Saudi Hizballah, anasakwa kwa kuhusika kwake kwenye shambulio la bomu la mwaka 1996 dhidi ya jengo la Khobar Towers karibu na Dhahran, Saudi Arabia.
Mnamo tarehe 25 mwezi Juni, mwaka 1996, wanachama wa Saudi Hizballah walilipua lori la mafuta lililokuwa na vilipuzi vya plastiki kwenye maegesho ya Khobar Towers, jengo la makazi lililotumika kama makazi ya wanajeshi wa Marekani. Mlipuko huo nusura uliharibu kabisa jengo lililokuwa karibu, likawaua wanajeshi 19 wa Marekani na raia mmoja wa Saudia, na ukawajeruhi mamia ya watu kutoka mataifa mbalimbali.
Mnamo tarehe 21 mwezi Juni, mwaka 2001, jopo kuu la mahakama ya serikali kuu lilimfungulia rasmi mashtaka al-Nasser na watu wengine 13 waliohusishwa na shambulio hilo.
Mnamo tarehe 12 mwezi Oktoba, mwaka 2001, Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje ya Marekani ilimtaja al-Nasser Gaidi wa Kimataifa Mwenye Sifa Maalumu kuambatana na Amri ya Rais 13224, kama ilivyorekebishwa. Matokeo ya kutajwa huku, miongoni mwa matokeo mengine, ni kwamba mali yote na maslahi ya al-Nasser katika mali, vyote vilivyoko chini ya mamlaka ya Marekani vimezuiwa, na watu wa Marekani kwa jumla wamekatazwa kushiriki kwenye miamala yoyote na al-Nasser. Yupo pia kwenye Orodha ya FBI ya Magaidi Wanaosakwa Zaidi.
